Skip to main content

Barua Kutoka Gerezani Kuhusu Maisha Na Mafanikio

#TANO ZA JUMA #45 2018; Barua Kutoka Gerezani Kuhusu Maisha Na Mafanikio, Mteja Muhimu Ambaye Hupaswi Kumpoteza, Fedha Ni Zao La Hamasa Na Ijue Thamani Ya Muda.

Rafiki yangu mpendwa,

Juma jingine la mwaka huu 2018 linaelekea kutuacha, ni juma namba 45, juma ambalo nina hakika limekuwa bora sana kwako, kwa sababu umejifunza, umechukua hatua na umepata matokeo ambayo yamekufundisha zaidi au kukupa hamasa zaidi.

Kumbuka kwenye maisha hakuna kushindwa mpaka pale unapoamua kukata tamaa mwenyewe. Haijalishi umekutana na magumu kiasi gani, kama bado upo tayari kuendelea, bado unayo nafasi ya kufanikiwa zaidi. Ni swala la muda tu na utapata kila unachotaka kupata.

Muhimu ni wewe udhibiti kile unachoweza kudhibiti na kuachana na vile visivyo chini ya udhibiti wako. Na kitu cha kwanza unachoweza kudhibiti, ambacho unapaswa kukipa kipaumbele ni hatua unazochukua wewe mwenyewe. Pia kitu ambacho hakipo kwenye udhibiti wako ni matokeo unayopata, usiumizwe nayo sana, wewe kazana na hatua unazichukua na utazidi kupata matokeo bora zaidi.

Karibu kwenye TANO ZA JUMA, ambapo nimekuandalia mambo matano muhimu sana kwako kujifunza na kuchukua hatua ili maisha yako yawe bora sana. Karibu ujifunze, utafakari jinsi haya yatakufaa kwenye maisha yako kisha uchukue hatua, kwa sababu kujifunza bila ya kuchukua hatua ni kupoteza muda na maisha yako.

#1 KITABU NILICHOSOMA; BARUA KUTOKA GEREZANI KUHUSU MAISHA NA MAFANIKIO.

Katika vitabu nilivyosoma juma hili, kimoja wapo kinaitwa THE BORON LETTERS, ambao ni mkusanyiko wa barua ambazo baba aliziandika kwa mtoto wake. Mwandishi wa barua hizi, Gary Halbert alikuwa mwandishi bora kabisa wa matangazo, na hivyo alichukua muda wake kumshirikisha mtoto wake yale yote aliyojifunza kwenye maisha, kuanzia kuwa na afya bora, kupata fedha na hata kuandika matangazo bora.

Barua hizi aliziandika akiwa gerezani, lakini kwenye kitabu haikuelezwa kwa nini alikuwa gerezani na alikaa kwa muda gani. Kwenye kitabu hiki, ameshirikisha barua 25 ambazo zina masomo mengi mazuri kuhusu maisha na mafanikio. Hapa nimekuchambulia yale muhimu sana, ambayo wewe rafiki yangu unaweza kuyatumia kupiga hatua zaidi kwenye maisha tako.

KUHUSU AFYA;

1. Kazi ya barabarani.

Mwandishi anamshirikisha mtoto wake kitu anachokiita kazi ya barabarani, kwa kiingereza ‘road work’, mwandishi anaandika kazi ya barabarani ni kutembea, kukimbia au kuwa na mchakamchaka. Mwandishi anamwambia mtoto wake anapaswa kufanya mazoezi ya aina hiyo angalau kwa saa moja kila siku, kasoro siku moja ya wiki, ambayo kwa mwandishi ilikuwa siku ya jumapili, siku ambayo alikuwa anafunga.

Pia anaandika muda mzuri wa kufanya mazoezi haya ni asubuhi. Anasema unapoamka, nawa uso, safisha kinywa kisha kula kipande cha tunda, kama ndizi na ingia barabarani. Nenda kwa nusu saa kisha rudi kwa nusu saa na utakuwa umekamilisha mazoezi yako ya siku. Hii itakupelekea kuwa na afya bora.

2. Umuhimu wa kufunga.

Mwandishi pia anamshirikisha mtoto wake umuhimu wa kufunga siku nzima mara moja kwa wiki. Anaandika kwa kufunga siku moja kwa wiki, inaufanya mwili ujiweke sawa. Pia siku ya kufunga anaandika usiwe na mazoezi makali au kazi nzito.

Mwandishi pia anamwonya mtoto wake kwamba asiwatangazie watu kwamba anafunga, maana wataanza kumpa maoni ambayo siyo sahihi, yeye afanye kimya kimya.

3. Kuhusu chakula.

Mwandishi anaandika chai siyo chakula muhimu cha siku, badala yake anamwambia mtoto wake atumie matunda asubuhi na kuendelea kula kiasi kidogo cha matunda mpaka muda wa chakula cha mchana. Anasema unapaswa kula angalau vipande vitatu vya matunda, na anapendekeza ndizi, chungwa na tufaa yasikosekane.

Anaandika chakula kiwe na kiasi cha wanga, lakini pia mtu apate protini ya kutosha na kupata kikombe cha maziwa kila siku. Maziwa yanampatia mtu madini ya kalshamu na kiasi kidogo cha protini. Protini zaidi inapatikana kwenye nyama.

4. Umuhimu wa kuwa na mwili imara.

Mwandishi anamwandikia mtoto wake kwamba moja ya jukumu lake kubwa kwenye maisha ni kuwa na mwili imara, hivyo mazoezi ya kuimarisha mwili ni muhimu. Anasema mwili unapokuwa dhaifu, au unapokuwa umezidi uzito, unatoa ujumbe kwa wengine kwamba hujali mwili wako na hivyo hawakuheshimu.

Mwandishi anamwambia kijana wake ajenge msuli, siyo tu kwa ajili ya mwonekano, bali pia kwa ajili ya heshima, anamwambia mtu mwenye msuli hachokozwi hovyo hovyo na hivyo msuli wake unamwepusha na matatizo madogo madoto.

Mwandishi anasema asili huwa ina tabia ya kuonea viumbe dhaifu, hivyo kama mwili wako utaonesha udhaifu, kila mtu atakuonea. Na hata magonjwa huwa yanashambulia miili dhaifu.

KUHUSU FEDHA.

5. Siri namba moja ya kupata fedha.

Mwandishi anasema kama akiulizwa ipi siri namba moja ya kupata fedha atajibu hamasa na mapenzi. Anasema mtu anapaswa kufanya kile anachopenda kufanya, kile ambacho anahamasika kukifanya, na hapo ndipo mtu anaweza kupata fedha nyingi atakavyo.

Mwandishi anasisitiza kwamba fedha ni zao la hamasa, kama mtu anapenda kuwa msanifu majengo, hapaswi kukimbilia kuuza majengo kwa sababu amesikia kuna fedha. Fedha zipo kule ambapo hamasa ya mtu ipo.

Anamsisitizia sana hili mtoto wake na pia anamwambia hata anapoajiri, asiangalie tu mtu mwenye sifa anazotaka, bali pia aangalie hamasa ambayo mtu anayo. Kama mtu hana hamasa kwenye kufanya kazi anayopewa, hapaswi kuajiriwa.

6. Mtazamo ni muhimu zaidi.

Mwandishi anasema, inapokuja kwenye kutengeneza fedha, basi mtazamo una nafasi kubwa sana. Mtazamo wa mtu ndiyo utakaomwezesha kutengeneza kipato kizuri au kumzuia asiwe na kipato kizuri.

Anamsisitizia mtoto wake kuwa mwanafunzi wa masoko na siyo mwanafunzi wa bidhaa. Fedha zipo kwenye masoko, ukiweka akili yako kwenye soko, kwa chochote unachofanya, utaweza kupata fedha.

7. Tafuta kundi lenye njaa kali.

Mwandishi anamwambia mtoto wake kwamba katia kuingiza kipato, hasa kupitia matangazo na hata biashara, unapaswa kutafuta kundi ambalo tayari lina njaa, kisha unauzia kundi hilo chakula. Mtu wenye njaa hasa, atanunua chakula kwa namna yoyote ile.

Mwandishi anasema watu wengi wanakosea kwa kuanza na bidhaa kisha kutafuta soko, yeye anasema anza na soko kisha tafuta bidhaa. Anasema ukishakuwa na soko, ukishakuwa na watu wenye uhitaji, hutakosa kitu cha kuwauzia. Lakini ukianza na bidhaa, utatumia nguvu kubwa sana kupata soko.

Kwa maneno mengine tunaweza kusema anzia sokoni, kwa biashara yoyote unayofanya au unayotaka kufanya, anza kwa kuangalia uhitaji ambao tayari watu wanao, kisha njoo na suluhisho, kazi itakuwa rahisi kwako kuliko ukianza na suluhisho halafu uanze kutafuta wanaolihitaji.

KUHUSU UANDISHI WA MATANGAZO.

8. Sheria ya Halber kwenye masoko.

Mwandishi anamshirikisha mtoto wake sheria ambayo amekuwa anaitumia kwenye masoko na kufanikiwa; WAUZIE WATU KILE WANACHOTAKA KUNUNUA.

Anasema sheria hii iko wazi na ni rahisi, lakini watu wanapenda kufanya mambo kuwa magumu. Anasema angalia watu wananunua nini kwa sasa kisha wauzie hicho. Kwenye uandishi wa matangazo, anamwambia mtoto wake aangalie matangazo yenye mafanikio makubwa na hayo yana kitu ambacho watu wanataka.

Pia anamwonya mtoto wake kuhusu tafiti na maoni ya wateja, anasema mara nyingi kile watu wanachosema siyo wanachofanya. Hivyo anamwambia mwanaye, asiangalie watu wanatumiaje midomo yao, bali aangalie wanatumiaje pochi zao.

9. Kanuni ya kuandika tangazo linalovutia wateja kununua.

Mwandishi anamshirikisha mtoto wake kanuni ya kuandika tangazo linazowavutia wateja kununua. Tangazo hilo lazima liwe na vipengele vinne;

Kipengele cha kwanza ni kushika umakini wa mteja, lazima limfanye mteja aache kile anachofanya sasa na kusoma au kusikiliza tangazo hilo.

Kipengele cha pili ni kumvutia mteja, lazima kile kinachotangazwa kimvutie mteja, kihusiane na mahitaji yake na aone kinamfaa.

Kipengele cha tatu ni kuibua tamaa ya mteja, hapa lazima mteja atamani sana kupata kile ambacho kinatangazwa.

Kipengele cha nne ni kumshawishi kuchukua hatua ya kupata kile anachotaka. Lazima mwishoni mwa tangazo kuwepo na ushawishi na maelekezo ya jinsi ya kuchukua hatua ili kupata kile kinachotangazwa.

Mwandishi anasema kanuni hii ikifuatwa vizuri, wateja watakuwa tayari kununua.

10. Fanya wanachofanya waliofanikiwa.

Mwandishi anamshauri mtoto wake jinsi ya kufanikiwa kwenye uandishi wa matangazo, anamwambia kwa mizuri minne mpaka mitano, kila siku aangalie matangazo yaliyofanikiwa sana, kisha ayaandike kwa mkono wake mwenyewe. Aandike neno kwa neno.

Kwa kuandika, mwandishi anasema, kunafanya ule uandishi wa matangazo yenye mafanikio kuingia kabisa ndani yako. Ni kama unanakili kanuni ya mafanikio kwenye akili yako. Ukifanya hivi kwa muda mrefu, akili yako inajifunza kuja na mawazo bora ya kuandika matangazo.

11. Una nafasi moja tu ya kumridhisha mtu.

Mwandishi anasema kwenye maisha una nafasi moja pekee ya kumridhisha mtu, na ukishachezea nafasi hiyo hupati nafasi nyingine.

Kwenye matangazo, anasema msomaji anafanya maamuzi ya kama atanunua au la kwa mwonekano tu wa tangazo, hata kabla hajasoma. Hivyo anamsisitiza mtoto wake kupangilia vizuri matangazo yake na uandishi uwe unavutia, kiasi kwamba mtu anapenda hata kabla hajasoma.

Kadhalika mwandishi anasema hata kwenye usaili, watu wanafanya maamuzi ya kama watamwajiri mtu au la kwa mwonekano tu wa nje, kinachofuatia baada ya hapo ni kutafuta sababu za kwenda na maamuzi yao ya awali. Yaani kama ulimvutia mtu alipokuona mara ya kwanza, ataanza kuangalia tabia na sifa zako nzuri ili ajiridhishe kukuajiri. Lakini kama kwa mwonekano wa kwanza hukumvutia, kwenye usaili mzima atakuwa anaangalia tabia na sifa zako mbaya ili ajiridhishe kutokukuajiri.

Mwandishi anasema tutumie vizuri sana nafasi ya kwanza tunayoipata, maana hatuipati mara mbili.

12. Epuka kufanya maamuzi katika hali hizi nne.

Mwandishi pia anamshirikisha mtoto wake makosa ambayo amewahi kuyafanya kwenye maisha yake, na mengi aligundua aliyafanya akiwa kwenye moja ya hali hizi nne. Hivyo anamwambia mtoto wake asifanye maamuzi yoyote anapojikuta kwenye moja ya hali hizo nne;

Moja; hasira

Mbili; njaa

Tatu; upweke

Nne; uchovu.

Anasema ukiwe kwenye hali yoyote katika hizo nne, maamuzi utakayoyafanya hayatakuwa bora kwako.

Badala yake anasema unapogundua upo kwenye hali yoyote katika hizo, fanya kitu kitakachoufanya mwili uwe na kazi, labda kutembea, kukimbia, kuandika au kuongea na wengine. Epuka kufanya maamuzi kwenye hali hizo nne.

13. Hatua saba za kufanikiwa kwenye uandishi wa matangazo;

Moja; tafuta soko la moto, watu ambao wapo tayari kununua.

Mbili; tafuta au tengeneza bidhaa ambayo tayari wanaihitaji.

Tatu; tengeneza tangazo linaloielezea bidhaa au huduma na faida ambazo mteja anapata kwa kuitumia.

Nne; jaribu tangazo hilo kwa watu 1,000 mpaka 5,000.

Tano; chambua matokeo uliyoyapata kwenye hatua ya nne.

Sita; kama matokeo ni mazuri, tuma tangazo kwa watu 20,000 mpaka 100,000.

Saba; kama matokeo bado ni mazuri, endelea kutoa tangazo hilo kwa watu wengi zaidi na zaidi.

Mwandishi anasema njia hizi saba ni rahisi, lakini watu huwa wanapenda kufanya mambo magumu na ndiyo sababu wanashindwa.

14. Tofauti kubwa kati ya wanaofanikiwa na wanaoshindwa.

Mwandishi anamwambia mtoto wake ipo tofauti moja kubwa sana kati ya wale wanaofanikiwa kwenye maisha na wale wanaoshindwa. Na tofauti hiyo ni UTAMBUZI. Anasema wanaofanikiwa wanajitambua sana, wanajua pale walipo, wapi wanaenda na wanajua wanafikaje pale. Kwa upande wa pili, wanaoshindwa hawajitambui, wapo wapo tu.

Mwandishi anasema lazima uwe unajua kila kinachoendelea kwenye kile unachofanya, lazima uijue misingi yote muhimu ya mafanikio kwenye kile unachofanya, lazima uwe na maarifa muhimu na taarifa sahihi. Pia mawasiliano na wengine waliopo kwenye tasnia hiyo ni muhimu.

15. Jinsi ya kupima kiwango chako cha utambuzi.

Mwandishi anamshirikisha mtoto wake njia ambayo yeye amekuwa anaitumia kupima kiwango chake cha utambuzi. Na njia hii ni kwenye kujua majira ya siku.

Mwandishi anamwambia mtoto wake, bila ya kuangalia saa aseme muda ni saa ngapi, yaani saa na dakika. Kisha aangalie saa na kulinganisha muda aliosema yeye na muda halisi. Anasema unapaswa kuwa ndani ya dakika saba za muda halisi, yaani kama muda halisi ni saa saba na nusu, basi bila ya kuangalia saa muda utakaoutaja uwe kati ya saa saba na dakika 23 mpaka saa saba na dakika 37.

Mwandishi anasema kama muda unaotaja bila ya kuangalia saa umezidi au kupunguza zaidi ya dakika kumi za muda halisi, upo chini sana kiutambuzi na unahitaji kuchukua hatua mara moja kupandisha juu kiwango chako cha utambuzi.

Njia ya kupandisha utambuzi wako ni kuacha unachofanya na kuwa na matembezi au kufanya chochote kitakachouweka mwili kwenye mwendo.

Rafiki, haya ndiyo mafunzo muhimu sana kuhusu maisha na mafanikio ambayo tunayapata kwenye kitabu cha THE BORON LETTERS, pata muda ukisome kitabu hiki, kina mengi sana ya kujifunza.

Pia anza kufanyia kazi haya tuliyojifunza hapa, hasa upande wa afya na fedha. Anza kazi ya barabara mara moja, kila mtu anaishi karibu na barabara, tenga saa moja asubuhi na mapema kwa ajili ya kukimbia, kutembea au kufanya mchakamchaka.

Muhimu zaidi, fanya kile unachopenda, fanya kile kinachokuhamasisha na kifanye kwa viwango vya juu sana, na kwa hakika fedha haitakuwa tatizo kwako.

#2 MAKALA YA JUMA; MTEJA MUHIMU AMBAYE HUPASWI KUMPOTEZA.

Rafiki, watu wengi wamekuwa wanahangaika kupata wateja wapya kwenye biashara zao, wanatumia kila mbinu ili kuwavutia waje. Lakini watu hao wanasahau wateja muhimu zaidi wa biashara zao, ambao wapo tayari kununua kama wakikumbushwa kidogo tu.

Juma hili nilikushirikisha makala muhimu kuhusu mteja muhimu wa biashara yako ambaye hupaswi kumpoteza. Kama hukupata nafasi ya kusoma makala hiyo, isome sasa hapa; Huyu Ndiye Mteja Bora Sana Wa Biashara Yako Ambayo Hupaswi Kumpoteza.

Pia nimekushirikisha makala kuhusu tatizo la fedha ambalo linawasumbua wengi na wewe pia, na jinsi ya kulitatua. Isome makala hiyo hapa; Tatizo Kubwa La Fedha Ulilonalo Wewe Ni Hili Hapa, Na Njia Ya Kulitatua Ipo Hapa.

Soma makala hizi na pia endelea kutembelea www.amkamtanzania.com na www.kisimachamaarifa.co.tz kila siku kwani kuna makala mpya na nzuri kila siku.

#3 TUONGEE PESA; FEDHA NI ZAO LA HAMASA.

Nimewahi kukuambia kwamba fedha ni kama mchumba mwenye wivu, mchumba ambaye anataka muda wote uwe naye, muda wote umfikirie yeye tu. Na mchumba huyu akigundua humfikirii na kumjali yeye anaondoka na kwenda kutafuta wengine wanaomjali na kumfikiria.

Hivi ndivyo fedha zilivyo, kama huna muda nazo hazitakuwa na muda na wewe. kama huzijali na kuzifikiria muda wote zitaenda kwa wale wanaojali na kuzifikiria.

Fedha ni zao la hamasa, chochote ambacho kinakuhamasisha, kile unachopenda kweli, kila ambacho unakifanya muda wote bila ya kuchoka, ndiyo kitu kitakachokuletea kipato kikubwa sana.

Hivyo rafiki, unapofikiria kuhusu fedha, anza kufikiria nini kinakupa hamasa sana, nini unapenda kufanya sasa kisha weka maisha yako yote kwenye kufanya hicho, na fedha hazitakuwa tatizo kubwa kwako.

Tatizo kubwa kwenye hili ni watu huwa wanakosa uvumilivu, wakiona kile wanachofanya kinachelewa kuwaletea matokeo wanayopata, na kuona wengine wakifurahia matunda ya vile wanavyofanya, wanajidanganya kule ndiyo kwenye fedha, wanaacha wanachofanya na kwenda kufanya vitu vingine. Wanahangaika sana, na hawapati fedha walizofikiria kupata. Na hata wakizipata, bado maisha yao yanakuwa na utupu fulani, kwa sababu kile wanachofanya siyo kinachowahamasisha zaidi.

#4 HUDUMA NINAZOTOA; PROGRAM MAALUMU YA UKOCHA KWA MWAKA WA MAFANIKIO 2018/2019.

Rafiki yangu mpendwa,

Nimeandaa programu maalumu ya UKOCHA kwa mwaka wa mafanikio 2018/2019. Mwanzoni niliandaa programu hii kwa wale walioshiriki SEMINA YA KISIMA CHA MAARIFA 2018, lakini pia naona inaweza kuwafaa wanamafanikio wote ambao wana vitu vikubwa wanavyotaka kufanyia kazi kwenye maisha yao.

Rafiki, kitu ambacho kinanihamasisha sana mimi, kitu ambacho napenda kufanya zaidi ni kuwashirikisha watu maarifa na kuwapa miongozo sahihi ya mafanikio. Pia napenda kwenda na watu bega kwa bega katika kufikia malengo yao makubwa. Na ndiyo maana nimekuwa na programu mbalimbali za ukocha. Hili ni eneo ambalo nazidi kuweka muda wangu mwingi.

Hivyo kama una lengo kubwa unalotaka kufanyia kazi kwa usimamizi na mwongozo wa karibu, kwa kipindi cha mwaka mzima wa mafanikio 2018/2019, wasiliana na mimi kwa ujumbe wa wasap 0717396253 ili tujadiliane zaidi namna programu hii itakavyokufaa.

Nafasi na programu hii maalumu ni chache, na zikishajaa sitaweza kuchukua watu wengi zaidi. Hivyo kama umeipenda, chukua hatua sasa kwa kutuma ujumbe kwa njia ya wasap 0717396253. Karibu sana rafiki tufanye kazi pamoja kwa mafanikio yako.

#5 TAFAKARI YA KUFIKIRISHA; IJUE THAMANI YA MUDA.

“Know the true value of time; snatch, seize, and enjoy every moment of it. No idleness, no delay, no procrastination; never put off till tomorrow what you can do today.” - Earl of Chesterfield

Ijue thamani halisi ya muda, kamata na kumbatia muda wako na furahia kila muda ulionao. Usiwe na uvivu, usiwe na uchelewaji na wala usiahirishe chochote. Usiache mpaka kesho kile ambacho unaweza kukifanya leo.

Rafiki, tumekuwa tunalalamika sana kwamba muda hautoshi, lakini nataka nikupe changamoto moja, na ifanye leo kisha nitumie majibu yako kwa wasap namba 0717396253.

Changamoto yenyewe ni hii;

Chukua karatasi na kalamu, upande mmoja weka orodha ya malengo na mipango yako yote muhimu kwenye maisha yako. Upande wa pili weka orodha ya kila kitu ulichofanya tangu juma hili kuanza, orodhesha kila kitu ulichofanya, kila uliyeongea naye, uliyewasiliana naye, usiache hata kimoja.

Kisha linganisha orodha hizi, kwenye kila ulichofanya, jiulize kinakusaidiaje kufikia malengo na mipango unayofanyia kazi. Kama kuna mtu ulibishana naye kwenye mtandao, jiulize je mabishano yako yanachangiaje kufikia malengo yako makubwa.

Fanya zoezi hili bila ya kujidanganya na nakuhakikishia utaona jinsi ambavyo umekuwa unapoteza muda wako wewe mwenyewe. Matokeo utakayoyapata kwenye zoezi hili, unaweza kunishirikisha kwa kunitumia ujumbe wa wasap 0717396253. Karibu sana tujifunze na kuchukua hatua sahihi kwa mafanikio yetu.

Rafiki, hapa kuna mengi sana ya kuondoka nayo, kwenye tano hizi a juma, ambayo kama utaanza kuyafanyia kazi kwenye juma tunalokwenda kuanza, utaweza kupiga hatua kubwa sana kwenye maisha yako. Jifunze na chukua hatua ili mwisho wa siku tuweze kukutana kwenye kilele cha mafanikio makubwa.

Makala hii imeandikwa na Kocha Dr Makirita Amani.

Dr. Makirita ni Daktari wa binadamu, Kocha wa mafanikio, Mwandishi na Mjasiriamali.

Dr. Makirita anaendesha mafunzo ya mafanikio kwa wale waliojitoa hasa kufanikiwa kupitia program ya KISIMA CHA MAARIFA.

Kama bado hujajiunga na KISIMA CHA MAARIFA, tuma sasa ujumbe wenye maneno KISIMA CHA MAARIFA kwa njia ya wasap namba 0717 396 253 (tumia wasap tu)

Kupata huduma nyingine za ukocha tembelea www.amkamtanzania.com/kocha

Kupata vitabu vizuri vya kusoma tembelea www.amkamtanzania.com/vitabu

Comments

Popular posts from this blog

WITO NI NINI?

MJUE ALIYEKUITANA KUMTUMIKIA WITO NI NINI? Kila mtu Mungu amemwita kwa nafasi yake amtumikie.Hata kama kwa nje wito utaonekana kufanana haina maana wito wa mtu mmoja na mwingine unafanana. Wito unatokana na kuitwa. Kila mtu Mungu amemwita amtumikie katika eneo Fulani.  Wito : Ni sauti au agizo analosikia mtu likimwelekeza nini cha kufanya.Katika wito wowote ukiwa umeitwa na Mungu atakuelekeza nini cha kufanya.Na unapoitwa na Mungu jitahidi kutenda sawa na wito wako ulivyo. NITAJUAJE NIMEITWA? 1.Utaisikia sauti ya Mungu ikisema na wewe: Kama kuitwa kwa kawaida kulivyo ndivyo mtu uisikia sauti ya Mungu  ikisema nae. Ebu angali mifano ya watu mbalimbali waliowahi kuisikia sauti ya Mungu ikiwaita kwa ajili ya kutekeleza agizo fulani. MUSA kabla ya kuanza kumtumikia Mungu alikuwa mchungaji wa mifugo ya mkwe Yethro kuhani wa Midiani.Katikati ya uchungaji Mungu alimwita Musa.Kumbe ili na wewe umtumikie Mungu unatakiwa uisikie sauti yake ikisema na wewe,Ni hatari sana kama uta

KIJANA NI NANI???

KIJANA NI NANI? NA MWANDISHI,  JANEROSA MAFWIMBO Neno kijana limekuwa na maana pana na linakuwa likipata tafsiri mbalimbali kutoka katika kila Taifa, jamii au tamaduni fulani. Kwakuzingatia mifumo au maisha ya jamii tunapata baadhi ya tafsiri za neno kijana kama ifuatavyo: Kijana ni mtu wa miaka 15-24. Hii ni tafsiri ya umoja wa Mataifa. Mathalani nchini Tanzania kijana ni mtu wa miaka 18-35 yaani baada ya balehe na mabadiliko ya maumbile toka utoto kuelekea ukubwa, aidha kw mujibu wa sera ya Taifa ya maendeleo ya vijana ya mwaka 1996 na kufanyiwa marekebisho mwaka 2007, inasema kijana ni mtu mwenye umri kuanzia miaka 15-24. Hivyo basi kijana ni mtu yeyote wa kike au kiume mwenye umri wa miaka 18-35 ambaye kwa mujibu wa mifumo ya kijamii au kitamaduni, kisiasa na kisheria anauwezo wa kujitegemea na kufanya maamuzi yake binafsi. Tofauti kati ya mtoto na kijana, wengi wanashindwa kutofautisha kati ya mtoto na kijana hasa waliopo katika elimu ya msingi na sekondari kutokana

MAMBO 12 YA KUFANYA UKIWA KIJANA

Vijana Tanzania Na Alfred Mwahalende Kwa mujibu wa mwandishi wa blog ya Dira Ya Kijana Tanzania  Janerosa Mafwimbo anasema “ Neno kijana limekuwa na maana pana na linakuwa likipata tafsiri mbalimbali kutoka katika kila Taifa, jamii au tamaduni fulani. Kwakuzingatia mifumo au maisha ya jamii tunapata baadhi ya tafsiri za neno kijana kama ifuatavyo: 1.     Kijana ni mtu wa miaka 15-24. Hii ni tafsiri ya umoja wa Mataifa. 2.     Mathalani nchini Tanzania kijana ni mtu wa miaka 18-35 yaani baada ya balehe na mabadiliko ya maumbile toka utoto kuelekea ukubwa, aidha kw mujibu wa sera ya Taifa ya maendeleo ya vijana ya mwaka 1996 na kufanyiwa marekebisho mwaka 2007, inasema kijana ni mtu mwenye umri kuanzia miaka 15-24.Hivyo basi kijana ni mtu yeyote wa kike au kiume mwenye umri wa miaka 18-35 ambaye kwa mujibu wa mifumo ya kijamii au kitamaduni, kisiasa na kisheria anauwezo wa kujitegemea na kufanya maamuzi yake binafsi. ” JE, UJANA NI NINI? 3.     Ujana ni hatua ambayo mtu anapi